NGUVU YA HABARI

Tuesday, December 8, 2015

Bodaboda Auawa Njombe



Dereva wa pikipiki Braison Mlonganile mkazi wa kijiji cha Nyumbo kata ya Ikuna mkoani Njombe ameuwa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali shingoni na watu wasiofahamika kisha mwili wake kutupwa mtoni.
Kutokana na tukio hilo jeshi la polisi mkoani humo lina washikilia watu watatu akiwemo mwanamke mmoja wakihusishwa na tukio hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari kamanda wa polisi mkoa wa Njombe Wilbroad Mtafungwa alisema kuwa mwili wa marehemu Braison Mlonganile umekutwa mtoni ukiwa na majeraha sehemu ya shingo yake.
Kamanda Mtafungwa alisema jeshi la polisi linatoa wito kwa raia kutojihusisha na matukio ya mauaji na kusema kuwa watii sheria bila Shuruti na kuwa watu wa kwanza kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo.

Wapateni Haki zao Watoto




Wazazi na walezi wametakiwa kuwapatia watoto wao haki za msingi ikiwemo elimu.
Selina Lyapinda ambaye ni mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali Mbeya Women Organisation Prevention of HIV and AIDs alitoa rai hiyo wakati akizungumza na blogu hii Desemba 08 mwaka huu.
Alisema baadhi ya wazazi na walezi huwakatisha masomo watoto wao kwa kuwatumia kama vibarua nafuu wa kuinua uchumia wao, vitendo ambavyo huwanyima watoto haki zao za msingi ikiwemo haki ya elimu.
Mmoja wa wazazi ambaye hakutaka jina lake litajwe alisema watoto walio wengi hutafuta vibarua wenyewe ili wapate fedha za kujikimu pamoja na kulipa michango shuleni ambayo wazazi wao wameshindwa kuimudu kutokana na ugumu wa maisha.
Wakizungumza na blogu hii baadhi ya watoto ambao wamejiingiza katika vibarua vya kukata majani ya mifugo wamesema walikatisha masomo yao baada ya wazazi wao kukosa fedha za kuwasomeshea.

Kayombo Kabutali Amshangaa Rais Dk Mgufuli



Kaimu Mwenyekiti Taifa wa Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA), Kayombo Kabutali amedai kuwa anamshangaa Rais John Magufuli kwa kupeleka sh. Bilioni 4 kwanye upanua wa barabara ya Mwenge jijini Dar es salaam huku baadhi ya Mikoa ikikabiliwa na baa la njaa.
Akizungumza na waandishi wa habari Kauli mjini Dodoma,
Kabutali alisema baadhi ya wananchi hawatanufaika na hatua hiyo kwa vile anaamini kuwa upanuzi wa barabara hiyo hautasaidia kutekeleza kipengele cha msingi cha haki za binadamu.
Aidha alisema kwa utaratibu huo, baadhi ya makundi ya wananchi hawatamuelewa hata kama utendaji kazi wake unakubalika.
Kibutali, alisema fedha hizo zingepelekwa mkoa wa Simiyu zisaidie familia zilizokumbwa na baa la njaa hasa akinamama na watoto wadogo ambao wamekosa msaada wa chakula baada ya wanaume kutelekeza familia zao.
Alisema rais alitakiwa atoe kipaumbele kwa baadhi ya Mikoa ambayo ina uhaba wa chakula ukiwemo Mkoa wa Dodoma.

Pius Mzimbe: Boresheni Miundombinu



Serikali imetakiwa kuboresha miundombinu ya barabara zinazoingia katika hifadhi za taifa ili kuongeza idadi ya watalii wa ndani na nje ya nchi wanaotembelea hifadhi hizo.

Rai hiyo imetolewa na Mhifadhi mkuu wa hifadhi ya taifa ya Kitulo iliyopo kati ya mkoa wa Mbeya na mkoa wa Njombe Pius Mzimbe wakati akizungumza na waandishi wa habari za Utalii na uwekezaji nchini(TAJATI) waliofanya ziara ya siku moja katika hifadhi hiyo chini ya ufadhili wa shirika la Wildlife Conservation Society(WCS).

Mzimbe amesema kuwa kumekuwa na idadi ndogo ya watalii wa ndani na pamoja na wa nje wanaofika kujionea vivutio vinavyo patikana katika hifadhi ya Kitulo kutokana na miundombinu ya Barabara kuwa mibovu.

Amesema iwapo kipande cha Barabara kutoka Chimala hadi Matamba chenye urefu wa kilomita 26 kitakuwa chini ya Wakala wa Barabara Tanroads itasaidia kuimarisha na kurahisisha watalii kufika kiurahisi  ndani ya hifadhi hiyo kuliko hivi sasa ambapo wengine wa watalii kurudia njiani hali ambayo huchangia serikali kukosa mapato.

Hifadhi ya Kitulo ilianzishwa mwaka 2005 lengo likiwa ni kutunza mandhari ya kipekee na makazi ya viumbe hai, kulinda vyanzo vya maji ya Mto Ruaha na Ziwa Nyasa na ni hifadhi ambayo ina vivutio ambavyo havipatikani katika hifadhi yoyote lakini pamoja na hayo imekosa watalii wa kutosha kutokana na miundombinu ya barabara inayokwenda katika hifadhi hiyo kuwa mibovu ambapo kwa mwaka hutembelewa na watali wasiozidi 700.


Wakazi Dodoma: Magufuli uko wapi?



Na Nazael Mkiramweni, Dodoma

Wakazi wa mkoa wa Dodoma wamemwomba Rais John Magufuli kufanya ziara ya kushtukiza kwenye ofisi za Mamlaka ya ustawishaji makao makuu (CDA) ili kujionea uonevu unaofanywa na mamlaka hiyo.

Walisema kuwa  moja ya uovu ni katika kuwanyang’anya wananchi ardhi yao bila kuwalipa fidia.

Ombi hilo limetolewa na wananchi hao wakati wakimpongeza Rais Magufuli kwa utendaji wake wa kazi ndani ya siku 30 alizokaa ikulu.
 Akizungumza kwa niaba ya wenzake Chifu Lazaro Chihoma alisema kuwa wakazi wa Manispaa ya Dodoma wana mategemeo makubwa na Rais Magufuli ya kuwasaidia ili waweze kupata ardhi ambayo wanaililia kwa muda mrefu bila mafanikio.
Alisema wafanyakazi wa CDA walipokuwa wanaanza kazi hawakuwa na usafiri hata wa baiskeli lakini ndni ya kipindi kifupi tu wameanza kuendesha magari ya gharama kubwa huku wakimiliki viwanja zaidi ya kumi huku wananchi wakiwa hawana viwanja hata vya kujenga nyumba.

 Naye Annarose Ngallya mkazi wa Kata ya Dodoma Makulu alimwomba Dk, Magufuli kuiangalia kwa jicho la huruma kata hiyo kwa kuwa ndiyo pekee ambayo wakazi wake hawajui hatma yao kufuatia CDA kutowapimia ardhi ya kujenga.

 Wakazi hao walisema endapo Rais magufuli hataingilia kati suala la mgogoro wa ardhi kati yao na CDA azma yake ya kuwapatia Wtanzania maisha bora haitafikiwa.

Naye Mussa Mloha ambaye ni mlemavu wa macho alisema kuwa itakuwa vyema kama Rais Magufuli atafika mkoani Dodoma kukagua idara mbalimbali kwa nako hali si shwari.